Pamoja

27 04 2007

Mbengu tulizopanda…

Kazi bure tul’ofanya,

Ukamwe mkono wa juu…

Twatazamana na wajukuu!

Pamoja tu kwenye jangwa…

Mawazo tele hamna raha,

Mawingu yatakapofunguka juu…

Mafuriko yatatubeba juu.

Ni nini tutakayofanya,

kuondoa yetu laana?

Mfano mzuri kurithisha

Pamoja tujitahidi…





Mwanzo Mpya

16 04 2007

Mwanzo mpya,

Matumaini mapya,

Mawazo mapya….

yaliyopita si ndwele,

lakini bila historia…

nisingeliona mbele.

Asanta kwako rafiki,

kwa kunionyesha…

ya muhimu duniani,

Kwanza,

kwa kunijulisha…

sie mie peke yangu,

ninayekimya na langu

Pili,

kwa kutumia m’da wako…

usiku kutwa hadi nikaelewa

mafunzo ya mababu zetu

tokea ujamaika,

hadi kisumu

Tatu,

kwa kunikumbusha…

utamu wa lugha,

Nne,

kwa kusisitiza

kuwa utu muhimu,

kuliko chochote kingine…

Na mwisho,

kuwa binadamu,

atofautishwa na wanyama…

kwani anapotaka kwenda msalani,

lazima aombe fursa kwanza!

kwani heshima si utumwa.





Jahazi likizama

14 04 2007

Jahazi likizama…

Utaruka we’ kwanza…

Au utan’tazama?

Utajuta ya zama…

Uliv’opoteza ujana?

Ya kesho utayawaza…

Au utamuachia Bwana?

Jahazi likizama…

Utaruka we’ kwanza…

Au utatazama,

Masilaha ya wenzio kwanza?





Pepo Kavu

7 04 2007

Mbona maisha kama pepo kavu?

Usin’ambie kila pepo na m’da wake,

ulimwengu ushanifunza….

Nini n’nalokosa lakini n’nachotamani?

Starehe ya kuketi na kupiga gumzo la kimaana…

Starehe ya kupiga gumzo na mtu aliyekomaa…

Chemchem la mawaidha yenye busara,

Mawazo tasa tukawa tumeyawacha nyuma…

Lakini ucheshi tusiutupilie mbali,

Mshindo wa bahari na mawimbi….

Kwenye miguu yetu tun’poketi ufukoni…

Hali ya anga likibadilika,

Maktabani au mkahawani sawa pia….

Sio kila siku mtandoni….

Niambie sasa,

Ukavu huu utaisha lini?

mchezo wa kuwindana sina mda nao…

tamaa uli’oamsha atautekeleza nani?

Yu wepi at’kaye zima kiu yangu?

Mwanya huu atauziba nani?