Mizizi Hatari

22 12 2006

Jenga nyumba yako
unavyotaka,
tumia udongo au matofali
makuti, mawe au glasi
jenga nyumba uwezano nayo
kifedha
kimuda
kisifa
jenga nyumba itakayo onyesha
ubinafsi wako

‘kisha jenga nyumba,
panda mti kando yake
mti ambao utafaidhika nao…
kwa matunda au kivuli,
au pahali ambapo
nyani na ndege
wanaweza tua na kupata riziki
kwa kukunyelea kichwani,
unapopumzika wewe
kivulini.

tend’keza nyumba yako
na utend’keze mti wako
lakini usisahau ukaupanda
mpakani mwa nyumba
kwa nini wauliza?

mizizi hatari
zitanyemelea polepole
na kubomoa nyumba’ko
sifa zote ul’zopata
zitapotelea kwenye kicheko
cha maadui, marafiki
majirani na hata wapita njia
“kafikiria nini yule?
hakujua mizizi hatari?”





ukoloni mambo leo

19 12 2006

nawaza nikiwazua
ukoloni mambo leo
keti nawe mwenzangu
ujaze mapengo haya
bila kuona haya

ukoloni mambo leo
fadhili au fadhila
tenda wema uende zako

ukongwe kabla uchumba
utumwa bila ujima
fafanua mwenzangu
nurisha walio gizani

kitambulisho kiplastiki
usiukose mfukoni
la sivyo rahisi sana
kutiwa mbaroni

centi vile vile, plastiki
usikose mfukoni
la sivyo
utajikuta kwenye dhiki

nyuso za plastiki
cheka nami n’cheke nawe
ukoloni mambo leo
um’kupata nawe?