Dad…

6 07 2008

My bags were already packed,

Looking foward to spending my hols…

with you and Mama.

But Alas! tis not to be,

You’ve left for somewhere…

I can only dream of.

 

I bid thee farewell Dad…

And find comfort,

in your words of wisdom…

Your strength, your courage,

and the Love you showered on us.





Je wajua?

18 06 2008

Penzi halilazimishwi, ni mtu kwa mtu wake.





Midundo ya Maisha

12 06 2008

Nina furaha leo kuwajulisha kuhusu Serina na Nje na Ndani…miradi mipya itakayowaletea mengi kuhusu maisha… Nje na Ndani itazungumuzia maswala ya afya na Serina itazungumuzia mambo kadhaa amabayo hayapati nafasi hapa. Karibuni.





Web Developer

9 06 2008

Natafuta Web-developer mwenye ujuzi wakutosha kwenye css na javascript. Ukiwa kazi ya kuunda waiweza au wamfahamu mtu anayeiweza, tuma barua pepe pamoja na viunganishi vya kurasa ulizounda kwenye anuani hii.





Masaibu

1 06 2008

Nina masaibu…

Sina amani ndugu…

Kichwa chaniuma,

Lakini moyo wangu zaidi wauma.

Ni wapi nitatua mzigo wangu?

Mzigo niliorundikiwa na wengine…

Kwa kutoweza kubeba wao…

Ni kama kaa moto…

Halishikiki mkononi.

Ni lini nitapata amani?

Wakati nimezingirwa na vita..

Ni nani atakaye nibembeleza ninapolia…

Kutokana na ugumu wa dunia?

Machozi yatiririka…

Na kuwacha mitaro yasiofutika.

Hili simulizi langu.

Hili labda simulizi lako?

Hili simulizi la wengi…

Vijana na wazee…

na wote walio kati kama mie.

Kichwa chaniuma…

kutokana na mawazo,

Moyo waniuma…

kwa yote ninayotolea jasho.

Naumwa… kwa kweli.





Nim’pata

18 05 2008

Nim’pata nilichotafuta…

Nim’pata na roho imetulia…

Nim’tafuta na nim’pata.





Maisha Safari

17 03 2008

Kitoto kichanga…

Hukaribishwa na wengi,

‘kishezaliwa tu! safari huanza!

kuishi duniani mkondo wa kwanza.

Wengine safari, kwao huwa fupi…

waliobakia nao mola awanusuru!

kulingana na sheria za wengine ataishi

Hawezi chagua…

mlezi wake duniani,

Hawezi chagua…

kati ya ukafiri na dini.

Amri zifuatwe bila ubishi!

Sio wote hubahatika…Safari hii kuimaliza.

Wengine safari huwa fupi…

wengine ndefu…

wengine safari ya furaha…

wengine safari ya matatizo.

Kisha baleghe…

Uamuzi mikononi mwake…

atakavyoishi ye…

na wengine wanaouhusiano naye,

atakavyofanya ye…

atakavyojitetea jangwani.

Wengine wana safari ngumu…

iliyojaa majaribio na mahangaiko,

Wengine safari, starehe tupu!

Waishije maisha yako?

Wanungunika?

Watesa?

Wateseka?

Wayafurahia?

Kufa…

wengine hujipangia…

wengine hupangiwa…

Kaka husema,

Kuzaliwa bahati…

Kufa lazima.

Nd’o maisha hayo!





Maiko*

3 03 2008

Leo nauvunja mtindo wangu wa mashairi maanake naandika kumhusu Maiko wangu ambaye ni mmoja wa watu wa kwanza kuyasoma mashairi yangu nilipokuwa bado kijana. Na nikishesoma kuhusu akina Stela na wengine wengi…wacha nami nimwage mtama kwenye kuku.

Ujana…ndio, ujana. Maiko tulikutana siku moja jioni, miaka mingi iliyopita kwenye ‘phonebooth’ huko Nairobi. Enzi hizo simu za viganjani hazikuwa zimejaa soko na simu za nyumbani zilikuwa zikipigwa vifuli na wazazi kwa hivyo vijana ilibidi tujue jinsi ya kulipia matumizi yetu. Sikumbuki nani alimtangulia mwenzake kutumia simu ile ya jamii lakini nakumbuka tulikuwa wawili tu! Mazungumuzo nayo sikumbuki yalianza vipi… siku hiyo tulizungumuza hadi mbalamwezi ukajitokeza, na tukaendelea kesho yake, na kesho yake na kesho yake…. Hatukuwa na gharama ya nauli au chochote kile maana tuliishi mtaa mmoja… bahati hiyo nakwambia!

Maiko ana sura ya kuvutia sana, na tabia ya kuvutia zaidi. Siku ziliendelea kupita na hisia zikaendelea kuongezeka. zawadi tulizounda wenyewe tulipatiana kwa mioyo iliyojaa upendo na kutaniana usiku kutwa. Tulikuwa na tabia wa kucheza mchezo wa ‘Scrabble’ hadi usiku wa manane na hamna hata siku moja tulipandishiana sauti kwa kukosana, Maiko ni mungwana kweli. Lakini ya maisha huwezi ukayapanga utakavyo wewe kila siku, Maiko hakuniambia kuwa anipenda kwa hivyo nikamchukulia kama rafiki. Matatizo yetu yakaanzia hapo maanake kuna rafiki yake mmoja aliyenisumbua tu kidogo nami nikakubali. Maiko kwa hasira naye akaanza kuonekana na rafiki yangu… kama ni wivu, nimeshauonja.

Hadithi yangu na Maiko ingeishia hapo lakini baada ya kuhamia uingereza, tukaanza kuwasiliana tena. Kwenye mawasiliano, sote tukaweza kuyabwaga manung’uniko yetu na kuweza kuwa marafiki kwa upya. Mawasiliano kwa miaka kadhaa ikawa kupitia intaneti na simu hadi majuzi nilipofika nyumbani.

Eeeh! ndio. Tulikutana jioni moja baada ya shughuli za siku kwenye mkahawa ‘The Mug’. Nilichelewa kidogo lakini kuingia hivi tu mkahawani, macho yakamwangukia Maiko, aliyeinuka na kunitupia tabasamu lake la kuua. Tukakumbatiana na kama si kuzingirwa na watu, bila shaka tungekumbatiana zaidi ya dakika hizo mbili. Tukaanza mazungumuzo na ikawa ni kama hatukuyakata miaka yote ile iliyopita… Maiko amebadilika, tena kwa njia nzuri.





Nyuma ya komputa

19 02 2008

Hapa nyuma ya komputa

Da’ mmoja na ukuta

Nywele sijazitana

Mavazi hayajapatana

Vipodozi havijaambatana

Manukato ni ya jana

Hapa nyuma ya komputa

Mengine mengi yanakolea

Kujificha nyuma ya maneno

yanifanyana nipige nderemo

Ni jinsi ya kuishi na vitetemeko

bila kubabaishwa na vitisho

Urembo wa sura

Ni laana najua

Maumbile yakishakaguliwa

Kwenye pipa watupiliwa

Hapa nyuma ya komputa

Uhuru wangu naupata.





Je wajua?

18 02 2008

Mtaka cha mvunguni sharti ainame.





Nipo

4 02 2008

Nipo nyumbani kwenye shughuli kidogo. Kumetulia jijini lakini vijijini bado.





Kimya

21 12 2007

Kukimya kwangu…

sio kumaanisha sina la kusema

maoni sitaki tu kutema

macho zaidi yan’tazama

Kukimya kwangu…

sio kumaanisha maneno sina

hotuba si neno geni ni tabia

moyoni hata hivyo najiimbia

Kukimya kwangu…

sio kuwa wa kusema nae sina

usifikirie kuwa ni ujinga

na tena ujue sio kuringa

Kukimya kwangu…

sio kumaanisha sijui nitamke vipi

bado sijafungwa ulimi

macho nayo bado usingizi

Kukimya kwangu…

ni njia ya kujifunza tena nakwambia

masikio niliyojaliwa yanapata kusikia

walio na lakunena nafasi nawapatia

Kukimya kwangu…

najua ni unyonge wangu

na pia ni nguvu kwangu

hilo lako jibu mwenzangu

Kukimya kwangu…

ni kusema kwangu.





Zubeda

30 11 2007

Zubeda usimfiche…

Nishakubali nin’ mke mwenza…

mfikishe nyumbani…

anisaidie kufua…

kazi yake isiwe tu kuchafua…

mnapoenda kusakata rumba…

kisha unrundikie mie dobi wako.

Zubeda hana la kuhofia…

Mila za mababu zetu zam’tambua,

Kwa hivyo vigumu…

nimchome na maji ya moto,

Au nimcharaze…

kwa kumfuata mme wangu,

Au nimuitie gengi…

lim’bwage msituni.

Usiwe na aibu kuwa Zubeda…

wanaume wazuri sio wengi…

dume kwenye boma lazima ligurume…

na akiguruma twamskiza,

asipoguruma hutoroka mke…

‘Mazubeda’ huongezeka.

Kuwa Zubeda si kazi rahisi…

hutakuwa naye asilimia mia,

kipenda roho hula nyama mbichi…

lakini tena,

ujane utakapoasili akitangulia ye

hutakuwa mjane peke yako…

wanetu watakuwa na damu moja…

ukikubali kuwa mke mwenza…

unakubali pia kuwa mlezi mwenza.

Zubeda,

Karibu tufahamiane…

Heri tujuane tukiwa wote tu hai,

kuliko wanetu kulezwa

na ma kambo tusiyemjua…

tabia na sifa.

Karibu mke mwenza,

Simba ameguruma.





Mganga wangu

30 11 2007

Mganga wangu kaona naumwa…

kan’tamkia maneno matamu…

kan’onyesha ukarimu…

kan’punguzia maumivu.

Mganga wangu kanipa dawa…

kan’nyanyua fikira…

kan’ondoa hasira…

kanipa hamu ku*****

Mganga wangu kan’ganga…

kan’weka kwenye nafsi yake…

kan’fanya siwezi mtenga…

kan’wacha kwenye njia panda.

Mganga wangu, mzazi mwenza…

kan’fungulia moyo wake…

kan’ambia kuwa penzi lake halifi…

nitamzika ye’

au

atanizika mi’

Mganga wangu, babake…

usiwakere mababu we!





Ninyunyizie mae

1 11 2007

Ninyunyizie mae…

Joto lin’ondoke

Ninyunyizie mae…

kutuzi un’ondoze

Ninyunyizie mae…

matawi nitawanye

Ninyunyizie mae…

tone hal’kufu

Ninyunyizie mae…

Upeo niupae

Ninyunyizie mae…

Nipe uhai





Rafiki

24 10 2007

Rafiki…

narudia neno hili

polepole

nikionja utamu wake

n’natabasamu peke yangu

kwani najua kuwa

rafiki huyu…

ni rafiki wa kweli

milango mingi tum’pitia

madirisha vilevile

um’nisaidia kukusanya kamba zangu

na kuzifuma pamoja

mkeka um’pendeza

bila we rafiki

sijui ungefanana aje.

Rafiki…

n’natabasamu kwani

husiti

kuniambia ukweli ulivyo

yawe machungu

au

yawe matamu

na cha muhimu kabisa

wanipa sikio lako

iwe kwa dakika chache

au masaa kabambe

Rafiki…

washangilia nami

mazuri yanapotokea

na kuniliwaza

n’napopatwa na mazito

Rafiki…

nakupenda.





Asubuhi ya leo

23 10 2007

Asubuhi ya leo

nimeshuhudia ajali

Mwanamke kagongwa na gari

Alikuwa amepotea mawazoni

Aitazama simu

Badala ya kutazama aendako

Breki hizo!

Kilio hicho!

Sitasahau maishani mwangu…

Asubuhi ya leo

N’nafurahia kuishi

Kupumua

Kupenda

Sina malalamiko

kumbuka

Asubuhi ya leo

ni wengi

hawajaiona.





Je Wajua?

11 10 2007

Maumbile si huja.





Upumbavu

4 10 2007

Mbona wanipasua moyo?

Kila dakika upo mawazoni…

Chochote nifanyacho,

nafanya kukufurahisha…

Mbona waniotesha ndoto

hadi mtindo unakuwa glasi moja kila siku?

La sivyo usingizi haunipati….

Mbona wanipandisha joto

kisha kunimwagia maji ya baridi?

Mbona ukanyemelea kwenye panya hili

Na kunifanya nikupende kikumbavu?

Mbona ubavuni kuna

Nafasi isiyojazika?

Lengo lako ushanieleza,

Najua wanitaka…

au wanitania?

Nami nakutaka…

Au nabahatisha?

Lakini

Mbona mambo ya dunia

magumu hivi?

Sisi sote wapumbavu sio?

Twajua tutokapo, hatujui tu tuendako.





Ike

29 09 2007

Leo nataka nimzungumuzie Ike…

Ike mwenye sauti ya kuvutia…

Ike aliyenifanya nicheke

karibu nimpige teke…

maana sikutaka kucheka kekeke

wakati mawazo ya ‘mme’,

yananiotesha mvi tele.

Ike nimemshinda kwa miaka…

ayajua ya malimwengu si mzaha!

Ike, Ike, Ike…

Asante kwa mda wako.





Mwiba

28 09 2007

Matembezi ya huku na kule

Wala hayendeki tena

Mwiba umen’dunga

Nimeshindwa kuutoa

Itabidi nitafute

Wa kuichomoa

 

Mazungumuzo na huyu na yule

Najua kuwa ni kero

Kuendelea na maisha

Kwani mwisho si leo

 

Hata bila viatu

Mtoni nitaenda

Kasiki nitalijaza

Kudungwa na mwiba

Ni jambo la kawaida





Kikomo

4 09 2007

Kutokana na mambo kadhaa, blogu naiweka kando kwa sasa…Serina.





Je wajua?

29 08 2007

Maji ya moto hayaunguzi nyumba…





Kila…

20 08 2007

Kila kukicha shughuli zaniita…

Shughuli lazima, huondoa mawazo.

Kila niangaliapo wadoya wako wa’nifuata…

Nani? lini? wapi?, ripoti wataka.

Kila n’napokuwaza machozi yatirirka…

Kupendwa kum’geuka, kukawa kufungwa.

Kila simu inapolia moyo wanidunda…

Nisipojibu, usiku nitalala wapi?

Kila n’napozungumuza nawe moto wawaka…

Haki yako wasema, kutimiza zako haja.

Kila ukisemacho sikiamini wala…

Miaka imepita, mie tena si fala.

Kila nilalapo nakufikiria ulipo…

Kila niondokapo wanililia nirudi…





Omba maji

7 08 2007

Omba maji, ukiwa na kiu

Kiu kitakumaliza, ukilitazama kasiki…

Walitazama kasiki, mwingine anywa…

Mwingine akiyanywa, meza mate pembeni…

Mate ukimeza, koo labanwa…

Koo kubanwa, kiu kuzidi…

Kiu kikizidi, mdomo wakauka…

Mdomo ukikauka, utashindwa kutamka…

Kushindwa kutamka, kujichimbia kisima…

Kisima cha hisia, machozi ya hasira…

Machozi ya hasira, wote watasikitika…

Ukiwa na kiu , omba maji jameni!





Wadhani Um’fika?

4 08 2007

Usimwone kafunga kanga…

Ukadhani umefika,

Usimwone mja mzito…

Ukadhani umefika.

Usimringie mwanadada…

Ukidhani umefika,

Usimwonyeshe madharau…

Akaja akapinduka!

Akitupa jicho kwingine…

Usidhani umefika,

Akimpa riziki mwingine…

Ujue bado hujafika.

Usikunje uso unapomwona…

Atajua hujafika,

Na usijaribu kukatisha kona…

Ukitaka we’ kufika.

Wahangaika…

Watatizika…

Na bado hujafika…

Usipotamka ukweli wako

Atajuaje amefika?





Heri niishi bila wewe

29 07 2007

Tafadhali zungumuza taratibu

Hata! sitosongea karibu

La sivyo watatusikia

Na kugundua kwanini sikuamini

Mapigo yakishekuwa desturi

Paza sauti mwenzangu

maanake sikio halisikii

Msamaha wamuomba nani

Asiyelala genezani

Kutokana na wako shetani

Wasiwasi unanizunguka

Ni wapi nitapindukia

Unachotaka sikupatii

Kuna mengi hatujayatatua

Kabla mme sijakutii

Mda wetu ulipotelea wapi

Kipenzi ulinipenya vipi

‘Kaniwacha na utupu moyoni

N’naogopa ushavunjika

Maanake sikuweza vumilia

Matumaini yashadidimia

Huwezi nishawishi

Na wala sitaki kujua

Presha sitaki ipande

Heri niishi bila wewe





Vitu nane msizojua kun’husu

23 07 2007

In’bidi niandike tena

Kwa kuwa um’nena

Vitu nane wataka kujua

Vitu nane nit’watambulia

Nimalizapo mi’ kusema

Zamu nanyi m’tapewa

Vitabu ni la kwanza,

hunionyesha mwangaza

Pili, napenda upekee

lakini sio upweke

Kujivunia upishi wangu namba tatu

kuridhisha wengine raha yangu

Nne, marafiki nawathamini

Bado sijajua ni kwa nini

Tano, useremala nim’jaribu

mbao nim’pasua bila aibu

Hata hivyo mazingira nayajali

namba sita sio kwa ajali

Nafasi ya saba naipa ndoto

maisha mazuri kwa wote watoto

La nane mjaze wenyewe

au tuseme tu ni uzembe

Watu nane … zamu yenu

Mwandani

Da Mija

Kitururu

Issa Michuzi

Ras Luihamu

Mentalacrobatics

Mwenye Macho

Ndesanjo (sio zile za Ethan…zingine)

na nane mkishewachagua

msisahau pia kuwajulisha





Pepo bado i kavu

12 07 2007

Jibu la Pepo Kato Sio Kavu, na Marazzmatazz

 

Vizuri umeketi ukadhamiri

Ya daftari pamoja na ya akilini

Kuwa ya dunia siyathamini

Na hamna yeyote ninayemwamini

Asilimia tisainitisa wala zaidi

Kweli usemavyo uchujaji naujua

Hisia zim’kuwa vigumu kuz’fafanua

Ulimwengu kanifunza roho yangu sitofungua

Hamna kama wewe anayenifahamu

Chanzo cha utesi wangu

Mashauri yenye faida bado natafuta

Gumzo na furaha bado zaniepuka

Hisia kuzibania sijui pakupinduka

Upweke, machozi wala hazijamwagika

Duh! Naona bado sijazinduka

Mawimbi baharini kun’ mazuri na mabaya

Kuvuma na kutulia kama waimbaji kwaya

Hupanda na hushuka bila kuelekezwa

Mengi zaidi ya hisia na ndoto sitazitaja

Daima ukavu usije’mi kunipata

Wasema ukavu huu si ukavu

Bali mfano tu kama vile ndoto

Nd’o maanake pepo kavu nikauita

Maana bado n’natumaini kuwa utapita

Mzibaji mwanya at’kapojitokeza

Hisia sizikatai wala sizikani

Majina kuyabandika wala si kazi

Nasubiri at’kaye kaa nami ufukoni

Mtandoni, maktabani na pia mkahawani

Najua siku itafika…lakini sijui lini

Ucheshi wako, utesi wangu

Duh! Kweli kama zamani





Demokrasia

28 06 2007

uchaguzi kidemokrasia…

yu wepi tuliyemchagua’si?

 

demokrasia yapeleka nchi mbele…

mafunzo ya wakoloni tushazoea,

bila demokrasia msaada ham’tapokea,

wafuateni wajuao njia msijepotea!

mwasema tuithamini demokrasia…

madawa hospitalini twasubiri,

msingi kwa vijana mliahidi,

barabara vijijini zafika lini?

endesha pajero demokrasia…

petroli gari wajaziwa,

nyumba kodi walipiwa,

masikini naye an’angalia!

lala hotelini demokrasia…

chokora si tatizo langu ’sha kwambia,

kazi yako si ulijichagulia?

niambie kingine kisicho gasia.

umoja ni nguvu twajivunia…

kura zenu mlinipa uhakika gani?

sie nyie mwajiita wapinzani?

mbona mwanililia’mi? Jameni!

majimbo kidemokrasia…

msiukaribie mpaka wetu!

msijichanganye na wakwetu!

msinitatize na shida zenu!!

kama demokrasia wapishe walioteuliwa….

wanichochea bahati haikuwa yako,

uchaguzi ujao labda zamu yako,

si demokrasia kwa wote?





Buriani

25 06 2007

Wakati umewadia

machozi hayatasaidia

moto umefifia

sikutaka kuuzima

mtindo wa maisha

buriani lazima





Sitarudia tena

15 06 2007

Wiki mwisho ukiwadia…

Sitaki riziki hata kufikiria!

Kazi mazoea kila jumaa kuisingizia,

kosa lile sitaki tena kulirudia.

Hadithi lile si la kukusimulia…

lakini wataka kujua mbona nalia.

Nyumbani upweke ul’kuwa mtindo nakwambia…

mtindo huo kuuvunja wiki mwisho ulikuwa.

Jumamosi usiku lazima nje nilitembea,

kuna binti moja mrembo niliyemchochea…

Jumapili asubuhi sikumbuki lilotokea,

hata jina la kwanza akilini ‘linipotea.

N’lipomtazama mjusi yule akijipodoa…

mawazo chungu tele, ni lini nil’potea?

Usingizi ul’nitoroka sebuleni al’potokea,

malipo ‘kaitisha haki yake ‘kaniambia!

N’na wasiwasi mdudu labda nim’uokota…

ulevi wangu mpira mbona sikuutumia?

Nyumbani upweke mtindo tena umekuwa…

Mwisho wa wiki sitaki tena kuutambua!





Wanifanyani?

13 06 2007

Uvumilivu wako…

wanifanya’mi mvumilivu,

Utu wako…

wanionyesha nia yako,

Ustaarabu wako…

wanipa joto,

Nguvu un’yoonyesha…

wanipa misisimiko,

Ucheshi wako…

wanipa raha,

Usamehevu wako…

wanipa amani,

Subira ulilo nalo…

wan’tuliza moyo.

Nakupenda lakini…

Umbali wako,

wan’chosha.





Raha ya pesa

9 06 2007

Mwisho mwezi keshafika,

wafanyi kazi wameridhishwa,

centi mikononi tele…

leo bibi hatapiga kelele.

‘Madamu’ tafadhali chukua taxi…

garama kwangu us’jali!

Majamaa njooni tupige raundi…

vilabu, bia na chagudoa, tuanzie wapi?

Raha ya leo mbona fupi imekuwa?

Ni matatizo tele si wajua…

Kimbia hapa, kimbia pale,

nunua hiki, nunua kile…

Watoto mavazi wan’hitaji,

karo shuleni si utani,

umeme ut’katwa usipowahi,

Bibi naye we! ni mkali!

Mashemeji nao mlangoni,

wezi nao ukingoni…

Sitoo chakula hata sijajaza!

Pesa nikiwa nawe sina raha!

Mboga chemsha na sima kiresheni,

‘bucha’ sipitii ila nifikishwe’mi kichinjoni…

Viatu bila rangi wiki mbili zishapita,

Gari nalo benki wenye mnada walishewaita.

Boi na yaya virago wash’funga,

Bibi kaniacha an’sema mie mjinga!

Mpangishaji naye kampu mlangoni keshapiga,

Pesa bila wewe sina raha!





Niite utakacho

5 06 2007
Niite binti fulani…

kwa maana uhusiano kati

ya wazazi wangu,

ndio kilichonileta duniani.

Niite mama…

kwa maana umeona,

sifa hiyo inanitosha…

ulezi wa wana

nd’o kazi ya kwanza.

Niite mwana…

kwa maana umri wako,

na busara ulionayo,

na kwa heshima kwako…

nitaaitika.

Niite mwanamke…

kwa maana una nia

ya kukiri kuwa

mimi sio mme.

Niite kipepeo nyeusi,

kwa maana najisifia

uhuru wangu,

na rangi yangu…

sitotupilia mbali historia yangu.

niite dada,

niite ndugu,

niite mpendwa,

niite mpenzi…

niite kafiri,

niite jasiri…

niite mzembe,

Niite utakacho…

kwa sababu unazozijua mwenyewe…

hautanibadili nilicho.





Mapumziko!

29 05 2007

Kisikusiku haujawahi kufika…

mchana bado haujaondoka,

ushatazama kivuli kwenye maji matulivu?

masiku nayo hupita hivyohivyo … kijivujivu.

Kekeo hajamaliza wimbo wake wa jioni,

Tayari wa asubuhi nausikia masikioni…

Moyoni nasononeka,

na tena nalalamika,

kuwa masaa hayasimami

nami nipate mapumziko…

Kwani siku hizi fupifupi

hazina mwisho?





Likizo

13 05 2007

Niko kwenye likizo,

n’tarudi si tatizo…

bora tu uhai





Pamoja

27 04 2007

Mbengu tulizopanda…

Kazi bure tul’ofanya,

Ukamwe mkono wa juu…

Twatazamana na wajukuu!

Pamoja tu kwenye jangwa…

Mawazo tele hamna raha,

Mawingu yatakapofunguka juu…

Mafuriko yatatubeba juu.

Ni nini tutakayofanya,

kuondoa yetu laana?

Mfano mzuri kurithisha

Pamoja tujitahidi…





Mwanzo Mpya

16 04 2007

Mwanzo mpya,

Matumaini mapya,

Mawazo mapya….

yaliyopita si ndwele,

lakini bila historia…

nisingeliona mbele.

Asanta kwako rafiki,

kwa kunionyesha…

ya muhimu duniani,

Kwanza,

kwa kunijulisha…

sie mie peke yangu,

ninayekimya na langu

Pili,

kwa kutumia m’da wako…

usiku kutwa hadi nikaelewa

mafunzo ya mababu zetu

tokea ujamaika,

hadi kisumu

Tatu,

kwa kunikumbusha…

utamu wa lugha,

Nne,

kwa kusisitiza

kuwa utu muhimu,

kuliko chochote kingine…

Na mwisho,

kuwa binadamu,

atofautishwa na wanyama…

kwani anapotaka kwenda msalani,

lazima aombe fursa kwanza!

kwani heshima si utumwa.





Jahazi likizama

14 04 2007

Jahazi likizama…

Utaruka we’ kwanza…

Au utan’tazama?

Utajuta ya zama…

Uliv’opoteza ujana?

Ya kesho utayawaza…

Au utamuachia Bwana?

Jahazi likizama…

Utaruka we’ kwanza…

Au utatazama,

Masilaha ya wenzio kwanza?

http://serina-serina.blogspot.com/2007/04/when-ship-sinks.html





Pepo Kavu

7 04 2007

Mbona maisha kama pepo kavu?

Usin’ambie kila pepo na m’da wake,

ulimwengu ushanifunza….

Nini n’nalokosa lakini n’nachotamani?

Starehe ya kuketi na kupiga gumzo la kimaana…

Starehe ya kupiga gumzo na mtu aliyekomaa…

Chemchem la mawaidha yenye busara,

Mawazo tasa tukawa tumeyawacha nyuma…

Lakini ucheshi tusiutupilie mbali,

Mshindo wa bahari na mawimbi….

Kwenye miguu yetu tun’poketi ufukoni…

Hali ya anga likibadilika,

Maktabani au mkahawani sawa pia….

Sio kila siku mtandoni….

Niambie sasa,

Ukavu huu utaisha lini?

mchezo wa kuwindana sina mda nao…

tamaa uli’oamsha atautekeleza nani?

Yu wepi at’kaye zima kiu yangu?

Mwanya huu atauziba nani?





Namlilia malkia

7 02 2007

Namlilia jirani,

Alikuwa malkia.

Kamkosea nani,

asiye na hisia?

Usiku wa juzi,

Kanieleza yote…

Jinsi aliv’ofikia uamuzi,

Kuwa kalemewa na vyote.

Chini ya mnazi…

Kapatikana Kesho yake.

Kazibwa mdomo,

hatukumsikia…

Kafungwa mikono,

hak’weza ‘jitetea…

Kachapwa viboko,

kawachwa kalegea…

Namlilia jirani,

malkia miongoni mwa malkia.





N’natumaini

24 01 2007

Kam’ kawaida,

kuwaza na kuwazua…..

nini kipya wauliza?

sina mapya…

matumaini tu!

N’natumaini kuwa u nuru yangu,

Utanionyesha njia wakati wa giza

Utanionyesha mbele n’napofika mwisho

Utaniliwaza n’naposhikwa na msiba

N’natumaini kuwa hutan’peleka mrama,

hata kam’ tum’gombana,

hata kam’ tum’koseana,

hata kam’ tun’ maswala ya kindani

yanayosababisha mapambano.

N’natumaini kuwa hut’nipa kamba,

un’ambie n’ende zangu.

Nim’pokea kamba nyingi maishani mwangu,

n’lizorundika kwenye sitoo,

nafikiria kushona mkeka

n’tauweka kwenye shoo.

N’natumaini matumaini yangu,

Hayat’kupa unyonge…





Mizizi Hatari

22 12 2006

Jenga nyumba yako
unavyotaka,
tumia udongo au matofali
makuti, mawe au glasi
jenga nyumba uwezano nayo
kifedha
kimuda
kisifa
jenga nyumba itakayo onyesha
ubinafsi wako

‘kisha jenga nyumba,
panda mti kando yake
mti ambao utafaidhika nao…
kwa matunda au kivuli,
au pahali ambapo
nyani na ndege
wanaweza tua na kupata riziki
kwa kukunyelea kichwani,
unapopumzika wewe
kivulini.

tend’keza nyumba yako
na utend’keze mti wako
lakini usisahau ukaupanda
mpakani mwa nyumba
kwa nini wauliza?

mizizi hatari
zitanyemelea polepole
na kubomoa nyumba’ko
sifa zote ul’zopata
zitapotelea kwenye kicheko
cha maadui, marafiki
majirani na hata wapita njia
“kafikiria nini yule?
hakujua mizizi hatari?”





ukoloni mambo leo

19 12 2006

nawaza nikiwazua
ukoloni mambo leo
keti nawe mwenzangu
ujaze mapengo haya
bila kuona haya

ukoloni mambo leo
fadhili au fadhila
tenda wema uende zako

ukongwe kabla uchumba
utumwa bila ujima
fafanua mwenzangu
nurisha walio gizani

kitambulisho kiplastiki
usiukose mfukoni
la sivyo rahisi sana
kutiwa mbaroni

centi vile vile, plastiki
usikose mfukoni
la sivyo
utajikuta kwenye dhiki

nyuso za plastiki
cheka nami n’cheke nawe
ukoloni mambo leo
um’kupata nawe?





Umen’pa moyo

26 11 2006

Mwenzangu,
hujanisahau
umen’pa moyo

Kila n’napokuwaza
unan’pa moyo

kazi un’yofanya
usiku na mchana
umen’pa moyo

jinsi unav’ong’ang’ana
kukuri kakara
umen’pa moyo

mlango wa kwanza
wa pili na tama
umen’pa moyo

kwa majaribio na raha
machache na mahaba
umen’pa moyo

kwa kun’chekesha na kun’tania
kunielekeza bila kuniangusha
umen’pa moyo

hili langu dua,
akubariki Mola,
na Akupe moyo.





Mwenzangu

30 10 2006

Bilauri kwenye sinia
hugongana
lakini
hazivunjiki
Penzi langu kwako
hivyo hivyo,
mwaka nenda,
mwaka rudi.
Miaka kenda na bado nahesabu

Najaribu kukusahau
tabasamu lako
mavazi yako
mwendo wako
Najaribu,
usiku na mchana
kuachana
kupatikana
na huzuni uliodua tulipoachana

Maji mengi yamepita
chini ya daraja
mengi,
masafi
machafu
mazito
cha muhimu
daraja bado lipo
na twasimama hapo hapo.

Penzi kikohozi
halifichiki
wajijua
mbona washuku